Marehemu Langa aliwahi kuimba kwamba “ukitaka kumficha
mwafrika weka ujumbe kwenye vitabu”. Langa alimaanisha kuwa sisi hatuna
tamaduni ya kupenda kupekua-pekua vitabu. Hili siyo jambo jema lakini kizuri Zaidi
ni kwamba hii tabia si ya kurisi kama tulivyorisi rangi zetu bali tunaweza
kubadilika na kuutengeneza utamaduni huu miongoni mwetu baada tu ya kutambua
umuhimu wake na kutengeneza mifumo ya kuwezesha hilo kutokea.
Binafsi naamini kupitia kusoma ni njia kuu ya kujitoa kwenye
matatizo tuliyonayo. Ukweli wa hili unajidhihirisha hata kwenye historia.
Kipindi mtu mweusi alipoishi kama mtumwa nchini Marekani ni kipindi ambacho pia
hakuruhusiwa kujua kusoma wala kuandika, sheria zao zilikataza kabisa mtu
mweusi kupelekwa shule na bwana wake. Walijua kabisa mtu yule alikuwa ana akili
na kama angejua kusoma basi hiyo ingekuwa kama tochi yake kuona yale
asiyotakiwa kuyaona na huo ungekuwa mwisho wa unyonyaji na ukandamizaji
ulioendelea. Hata vuguvugu la kutafuta haki za watu weusi lililetwa na wale
wachache ambao kwa bahati ya mtende waliweza kujua kusoma. Huko Afrika ya
Kusini pia makaburu walibana elimu kwa watu weusi ukilinganisha na wao wenyewe,
hata Mandela mwenyewe alipata elimu kwa sababu baba yake alikuwa mshauri wa
chifu na alipofariki alilelewa na chifu. Hata hapa kwetu wakoloni hawakutoa
elimu kwa faida yetu bali kwa faida zao pale ilipowabidi kama vile kusomesha
watoto wa machifu ili waelewane na machifu.
Mfano mkubwa kabisa katika kuonesha kusoma kunaweza
kubadilisha maisha ya mtu ni wa kijana mmalawi aitwaye William Kamkwamba.
Kamkwamba alizaliwa kwenye familia masikini huko kijijini kwao Masitala karibu
na jiji la Kasungu. Alipokuwa anaingia kuanza elimu yake ya sekondari, Malawi
ilikuwa imekumbwa na mafuriko yaliyoambatana na njaa kitu ambacho kilimfanya baba
yake ashindwe kumlipia ada ya shule. Kamkwamba alibaki nyumbani ila hakukaa tu
bali alipenda kwenda maktaba kujisomea ili angalau awe sambamba na wenzake
pindi ada itakapopatikana na akarudi shule. Alisoma vitabu mbalimbali ila
kilichobadilisha maisha yake anasema kiliitwa Explaining Physics ambacho kilieleza jinsi kata upepo inavyofanya
kazi na kutengeneza umeme. Kwa kutumia kitabu hicho aliweza kutengeneza kata
upepo kwa kuunga-unga kutoka kwenye vitu alivyookota jalalani likatoa umeme
akawasha taa kwao na akatumia kuchaji simu za wanakijiji. Aliwahi pia
kutengeneza bayogesi na pampu ya kuvuta maji kutoka kisimani japo
havikufanikiwa kutokana na kukosa vifaa. Cha ajabu shule za serikali za Malawi
zilipoombwa kumuingiza aendelee na elimu yake zilisema alikuwa ana umri mkubwa,
na hata serikali ya Malawi haikujua wala haikumsaidia chochote katika kukuza
kipaji chake; na hata alipokutana na raisi Bingu Wa Mutharika alipokuwa
amealikwa kwenye mkutano mmoja huko Afrika Kusini ndio ilikuwa mara ya kwanza
rais anamuona William na kwa mara ya kwanza anasikia habari zake. William
alipata scholarship kwenye shule ya international na baadae akaenda kusoma
African Leadership Academy kabla ya kwenda kusoma uinjinia chuo kikuu cha
Dartmouth nchini Marekani.
Wengi mara ya mwisho kusoma huwa ni pale tukiwa shuleni na
mara nyingi tunasoma field zinazotuhusu tu. Ni vigumu kumkuta mwanafunzi wa
udaktari labda anasoma kitabu cha historia, filosofia ama astrofizikia. Lakini
hatuwezi kuzungumza kuwa hatuna utamaduni wa kupenda kusoma bila kugusa upande
wa pili kwamba hatuna pia utamaduni wa kuuandikia umma (tunao wataalamu
wanaoandika sana machapisho ya tafiti ila ni katika kada zao za elimu, tofauti
na kuuandikia umma). Nikitembelea maduka ya vitabu, vitabu vingi ninavyoviona huwa
ni vya kujifunzia mashuleni na vingine
huwa vimetoka nje ya nchi ambavyo huwa vinawaelekeza watu jinsi ya kupata
mafanikio maishani. Vilivyoandikwa na watanzania wenzetu huwa ni kimoja kimoja
ukiachilia mbali vijitabu vyenye stori za watu wanaodai wamewahi kupelekwa
kuzimu na mambo mengine ya uchawi ambayo huwa ni uwongo tu. Huwa najiuliza kama
tunataka kujifunza kuhusu kufanikiwa katika mazingira ya kitanzania kwanini
watu kama akina Mo Dewji, Mengi ama Bakhresa wasituandikie tuyasome mawazo yao.
Kwanini wazee waliopata bahati ya kusoma enzi za mwalimu wasituandikie mawazo
yao kuhusu hali ya nchi inavyokwenda. Kwanini wanasayansi wachache tulio nao
wasituandikie kuhusu maendeleo ya sayansi ama nini kifanyike kuhusu sayansi
nchini kwetu. Watu waliofanikiwa kwenye sekta zao kama akina Platinums na
Samata waweza kuongea na wengine wanaotaka kuwa kama wao kupitia vitabu na sio
kwa kuwafollow tu kwenye instagram.
Ni dhahir pia hatujaweka mazingira mazuri yenye kuamsha
utamaduni wa kupenda kusoma. Tukijenga nyumba zetu nzuri za gharama tunaweka
sebure nzuri ili wageni watupe sifa ila tunasahau kuweka maktaba na kuzijaza
vitabu. Kama kuna kitu sijawahi kusikia serikali hata ikikiongelea huwa ni
maktaba zake, mara ya mwisho naingia maktaba ya mkoa wa mwanza ilikuwa mwaka
2011 ila vitabu vyake vilikuwa ni vya
muda mrefu vilivyochoka na kulikuwa na kiingilio. Wengi waliokuwa mule walikuwa
ni wanafunzi wa sekondari waliokwenda pale ili kupata utulivu wa kujisomea
mambo yao ya shuleni. Vitabu vingi huwa tunapewa kama misaada japo tuna watu
wenye uwezo wa kulipia watu mamilioni ya pesa waangalie mpira bure zaidi ya
mara moja. Kila mtaa wetu una banda la kuangalizia mpira unaorushwa kutoka
upande mwingine wa dunia na tunalipia ila hatuwezi kuweka hata ka maktaba cha
watoto wadogo. Mashuleni kwetu si tu kwamba watoto wanakosa vitabu vya
kujifunzia bali wakati mwingine hata mwalimu anakosa kitabu cha kufundishia
Mwaka 2013 nilipoona kuna ugumu wa kupata vitabu hapa nchini
nilisaidiwa na rafiki yangu kuagiza kifaa kwa jili ya kusomea kiitwacho kindle. Kilikuja bila kava na nikaamua
kulitafuta kava lake kwenye maduka ya jiji letu kuu la Dar es salaam. Nilishangazwa
pale nilipoona kuwa maduka yoote niliyotembelea yakiwemo ya kariakoo, mlimani
city, posta na kwingine hayakuifahamu kindle
na hawajawahi hata kuisikia. Mmoja kati ya wauzaji aliniuliza “unasema
unatafuta kinu?”. Ila jibu la kwanini kifaa hiki hakikujulikana kwenye maduka
haya miaka takribani 6 baada ya kuanza kutolewa na kampini la Amazon ni kwa
sababu hakina kazi nyingine zaidi ya kusomea tu. Simu za gharama zikitoka huwa
zinapatikana nchini ndani ya mwezi huohuo ziliotolewa. Tunaishi kwenye dunia ya
kiteknolojia zaidi ya wakati wowote duniani, na kitu muhimu ni nini kimo ndani
ya vichwa vyetu. Tutaweza kuendana na dunia hii kwa kupenda kuongeza ujuzi na
njia ya kufanya hilo ni kwa kusoma. Tukuze utamaduni wa kupenda kusoma.

