Saturday, 12 November 2016

PLACEBO



Naamini katika maisha yetu wote tulishawahi kusikia ama kufanya kitu ambacho tuliambiwa ni tiba pale tunapoumwa japo hakiingii akilini kuwa tiba. Nakumbuka nilipokua nakua ulikua ukipata kipele jichoni tulichokiita sekera uliambiwa ukaongelee kwenye tundu la choo na kitaisha, na kweli siku chahe baada ya kuongelea kwenye tundu la choo kipele kile kiliisha; niliambiwa pia jino liking’oka ili liote lingine basi sina budi kutupa jino lile lililong’oka batini, na kweli nilipotupa jino lingne liliota, na wale watoto wenye mapengo walikiri kutotupa meno yao batini; na mengine mengi.
 Image result for placebo
Nimekua nikiongelea baadhi ya tiba ambazo ni za uongo lakini najua kabisa kuna mtu akisoma anaona ninadanganya kwa sababu yeye amewahi kutibiwa na moja ya tiba hizo na akajiona kupona. Wote tunaowaona wakitoa ushuhuda kuhusu tiba ambazo ni za uwongo sio lazima wakawa wamepangwa na watoa huduma zile, wengine ni waaminifu ambao kweli baada ya tiba zile walijisikia kupona. Sio wote tunaowaona kwenye runinga wakifanyiwa maombi na kuanguka na kuanza kupata degedege wanaigiza, wapo ambao wanafanya vile kweli bila kuigiza. Naamini mnakumbuka wanasiasa walivyosimama mbele ya kamera na kusema wanajisikia kupona dakika chache baada ya kunywa kikombe cha babu, naamini walijisikia kupona kweli na walikua hawatudanganyi.

Yote hayo na mengine nitayataja yanaanguka kwenye neno la kilatini “placebo” ambalo tafsiri yake inafanana na msemo wa Kiswahili “kupaka mafuta kwa mgongo wa chupa”. Kwenye fani hii ya tiba neno placebo lina maana ya tiba ambayo ni ya uwongo ama isiyo na viwango lakini inampa mgonjwa unafuu. Hii ndiyo inayowafanya wanaotoa tiba za uwongo kuendelea kung’ara na kutajirika kwani wateja wao ni kweli kabisa wanajisikia vizuri wakipata huduma zao na watawatafuta popote.

Mtu wa kwanza kufanya tafiti kuhusu swala hili alikuwa mwingereza John Haygarth aliyekuwa daktari mstaafu, baada ya kuwepo kwa tiba iliyohusisha kutumia vyuma kufyonza maumivu kutoka mwilini kama vile sumaku inavyovuta vyuma, na wagonjwa walipona maumivu. Vyuma hivyo vilikuwa vimetengenezwa na madini ya gharama na kuifanya tiba hiyo kuwa ya gharama. Haygarth alichukua vyuma vilivyotumika kwa tiba hiyo na pia akatengeneza vingine ambavyo havikutumia madini kama yale ya vile vya tiba. Cha kushangaza wagonjwa walipona maumivu bila kujalisha wametumia vyuma gani. Haygarth alikuwa sawa kufikiri kwamba kilichowaponya wagonjwa sio vile vyuma ila ni Imani ya wagonjwa kwa vile vyuma.

Tafiti nyingine ilifanywa na Daktari bingwa wa magonjwa ya moyo alieitwa Leonard Cobb miaka ya 1950 kwa watu waliokuwa wana maumivu ya vifua kutokana na magonjwa ya moyo ambao kwa kipindi hicho walikuwa wanafanyiwa upasuaji wa kifua na kufungwa mshipa mmojawapo wa damu ndani ya kifua ili kuruhusu damu nyingi kwenda kwenye moyo na hivyo kuondoa maumivu. Cobb aliwaweka wagonjwa wake waliokuwa wanasubiri upasuaji katika makundi mawili;wa kundi la kwanza aliwapasua kifua na kuufunga mshipa huo kisha kukifunga kifua; wa kundi la pili aliwapasua kifua ila hakufanya kitu chochote na kuwafunga kifua ila aliwaaminisha kwamba amewafunga mshipa huo. Cha kushangaza ni kwamba makundi ypote baada ya upasuaji yaliripoti kutopata maumivu ya kifua kama ilivyo kuwa kabla ya upasuaji. Maumivu ya wagonjwa hawa hayakutibiwa na upasuaji bali na Imani ya wagonjwa juu ya upasuaji ule, hii ndio placebo

Placebo haipo tu kwenye tiba za uongo bali hata hospitalini ipo. Madaktari wawili wanaotoa tiba zinazofanana sio lazima waponye wagonjwa kwa kiasi kinacholingana, ndio maana upendo wa wagonjwa kwa madaktari tofauti haufanani. Lakini hospitalini kinachotokea ni kwamba juu ya tiba ya ukweli inayopatikana, placebo inaongezeka tofauti na tiba mbadala nyingi ambazo hazijathibitishwa ambazo huelemea kwenye placebo pekee. Tafiti zinaonesha kati ya mambo yanayoongeza uponaji wa mgonjwa juu ya matibabu yanayopatikana hospitalini ni kama vile kuvaa koti jeupe ukilinganisha na kuvaa t-shirt, kuongea vizuri na wagonjwa, umaarufu wa daktari n.k.

Inafikiriwa kinachosababisha placebo kuwepo ni kwanza kuzoea kuwa baada ya tiba huwa tunapata nafuu, kama vile mbwa waliozoeshwa kupigiwa kengele kabla ya chakula wanapotoa udenda hata tu wakisikia kengele; pili ni kiasi ambacho mgonjwa anaamini ataponywa na tiba fulani kinaendana na matokeo ya tiba yake; ama zipo sababu zaidi ya hizi ambazo bado hazijajulikana bado

Sayansi imeweza kuliona hili na njia za kuthibitisha tiba za kisayansi zimewekwa kiasi kwamba tofauti zinazoletwa na placebo zinafutwa kwanza na tiba inasimama kama tiba yenyewe. Kwa mfano kwenye sayansi tukitaka kujua kama dawa X inatibu maumivu ya mgongo tutawachukua watu wengi wenye maumivu ya mgongo na kisha tutaichukua dawa X pamoja na dawa nyingine inayofanana kabisa na dawa X na tutawapa wagonjwa wale. Wagonjwa wala wanaowapa dawa hizo hawatafahamu kama wanapewa dawa ya kweli ama ile geresha inayofanana nayo na wote watakuwa kwenye mazingira yanayofanana. Baadae tutaangalia ni kundi lipi lina wagonjwa wengi Zaidi waliopona maumivu ya mgongo. Watakaopona kwa placebo watakuwepo katika makundi yote hivyo watakaopona Zaidi ya hao watakuwa wameponywa na dawa ile.

Unaweza kushangaa kwani hata kama ni placebo swala si kupona tu! Lakini kuna hatari zinazoweza kuhusishwa na swala hili. Tafiti moja iliwachukua wagonjwa wa pumu na kisha kuwapa tiba mbadala na wakasema wanajisikia pumu yao imekwisha na wanapumua vizuri kabisa; lakini wakifanya vipimo, mapafu yao yanaonekana bado hayapo vizuri na wanaweza kubanwa pumzi muda wowote na hivyo hawashauriwi kuachana na dawa zao za kisasa. Kingine ni kwamba placebo ipo vizuri Zaidi kwa dalili kama vile maumivu, homa, uchovu na kukosa hamu ya chakula; hizi ni dalili ambazo zinaweza kuwepo kwa kuwa kuna ugonjwa mkubwa zaidi, maumivu yanapotulizwa na placebo huenda ikachelewesha kugundulika kwa ugonjwa uliopo.

Natumaini baada ya kujifunza haya hatutasimama kubishana kwamba tiba fulani ni tiba sahihi kisa tu sisi wenyewe ni mashahidi aidha tuliponywa nayo ama watu tunaowafahamu waliponywa. Njia sahihi ya kufahamu ni kama tiba hiyo imefanyiwa tafiti kisayansi na kukubalika.

1 comment: