UONGO KUHUSU UTOAJI
SUMU MWILINI
Neno SUMU limekuwa likitumika na matapeli kututisha kiafya
na kutufanya tununue bidhaa zao za uongo. Nadhani hata wewe katika pita-pita
zako umewahi kukutana na kikundi cha watu wakitangaza njia zao za kutoa sumu
mwilini na kuuza huduma hiyo. Wataanza kwa kutuelezea jinsi gani maisha yetu
yamezungukwa na sumu kuanzia vyakula, vinywaji, pombe, sigara, moshi wa magari,
madawa ya hospitali, hewa tunayovuta kwamba vyote hivyo vina sumu. Watasema
ndio maana siku hizi tunaumwa zaidi migongo, vichwa, mafua, n.k (hizi dalili
kila mmoja ameshawahi kuzipata) na wataongeza mengine ya kututisha kama
saratani. Baada ya hapo wataonesha bidhaa zao za kutoa sumu mwilini.
Wanaweza kumwaga maji yenye rangi kwenye chombo na
wakawaambia watu hiyo ni sumu na kisha wakachanganya na kemikali nyingine
ambayo inasababisha yale maji ya rangi kupoteza rangi na kuwa maji masafi,
“nunua hii dawa leo ujisafishe sumu mwilini mwako kama ulivyoona hapa”
watawaambia watazamaji walioshangazwa na kile kitendo. Lakini ukweli ni kwamba
hizi ni kemikali za kawaida tu ambazo zipo na kwa mtu aliyewahi kuhudhuria
darasa la kemia akiwa sekondari anaweza kukumbuka walivyokuwa wanachanganya
kemikali na rangi inapotea, na ninaamini zile dawa anazowauzia watu sio zile kemikali
anazochanganya. Wengine huwaambia watu kuingiza miguu kwenye maji na baada ya
muda maji yale yanabadilika rangi na hiyo rangi wanasema ni sumu inatoka kwenye
mwili ya aliyeweka miguu. Ukichunguza vizuri utakuta wamechomeka vichuma ndani
ya maji yale na wameunga kwenye chanzo cha nishati ya umeme mdogo; vyuma
vikidumbukizwa kwenye kemikali na vikapitishwa umeme basi vinalika na kama vina
kutu basi kutu itapukutika na maji yatachafuka, kwenye kemia hiki huitwa “electrolysis” na hakuna sumu yoyote inayotoka mwilini.
Watu wa tiba mbadala wameiba hili neno “utoaji sumu mwilini”
kutoka kwenye tiba ya kisasa, tiba ya kisayansi. Hospitalini utoaji sumu
mwilini hufanywa kwa watu waliokunywa sumu, waliozidisha kiasi cha dawa ama
pombe na katika hali hizi wagonjwa hawa huwa wanaumwa si utani.
Ni kweli tumezungukwa na kemikali nyingi, kemikali hizi
huenda zikawa ni za asili ama za kutengezezwa. Lakini miili yetu imeumbika
kujihami na kujisafisha na sumu ziingiazo mwilini kutoka nje pamoja na zile
inazotengeneza yenyewe. Maini yetu ndiyo kiungo cha muhimu kabisa ukiongelea
utoaji wa sumu mwilini, mafigo, mfumo wa chakula, mfumo wa upumuaji na mfumo wa
limfu vyote vinafanya kazi kuhakikisha sumu zinatolewa nje ya mwili.
Mtu anaekwambia ule vyakula fulani ili kutoa sumu mwilini
huo ni uongo, labda vyakula hivyo vikusaidie kwenye mambo mengine kiafya kwa
mfano matunda na mboga-mboga kwa wingi hutupunguzia uwezekano wa kuugua
magonjwa sugu. Ukikutana na mtu anakuuzia huduma ya kutoa sumu mwilini swali
lako la kwanza liwe “nitajie majina ya hizo sumu” na la pili liwe “sumu
hizo(hatozitaja maana hazipo) zinaletaje hayo magonjwa uliyoyataja?”. Matapeli
hawa huishia kusema tu SUMU bila kuzitaja majina yake na hakuna uhusiano wa
kile wananchoita sumu na magonjwa wanayoyasema yanatokana na hizo sumu.
Utapeli huu upo kwa kiasi kikubwa hapa kwetu kwani
nilipojaribu kuingiza maneno “utoaji sumu mwilini” kwenye google, taarifa zote
isipokuwa moja ya Wikipedia zilizokuja kwenye ukurasa wa kwanza ni taarifa za
uwongo zenye dhamira ya kumuuzia msomaji hizi juice na vifaa vya kudanganyishia
kutolea sumu mwilini, wataalamu wa afya hapa hatujafanya kazi yetu ipasavyo
kuielimisha jamii. Mitandao mingi ilionekana kuuza juice inaitwa TREVO ambapo
walisema nayo inatoa sumu. Kwenye mtandao wao wa trevocorporate.com wameandika
juice hiyo imetengenezwa na vitu vya asili 174 na inakupa: nguvu za ziada,
inakuongezea umakini wa akili, afya njema na kujisikia vizuri; wakaongeza
kwamba TREVO inasaidia katika: kupunguza uzito, afya ya moyo, afya ya seli(hii
sijui ni nini), afya ya mfumo wa chakula, mfumo wa fahamu, kinga ya mwili, afya
ya macho, mifupa na viungo, kuzuia uzee(naomba nirudie: kuzuia uzee) na afya ya
sukari kwenye damu. Tofauti ya hii na ile ya Loliondo ni hapa hakuna tu ndoto,
maana nayo kama inatibu karibia kila kitu. Hata mimi ningependa maisha yawe
rahisi hivi ila ukweli ni kwamba hayapo hivyo na natakiwa kusimama mbele ya
ukweli.
Usitishwe na vitu ambavyo havipo, kula vizuri, fanya
mazoezi, achana na tabia hatarishi kiafya, penda ku-check afya yako mara kwa
mara na ufurahie maisha kwani duniani si tunapita wote.
0 comments:
Post a Comment