Sunday, 18 September 2016

BODABODA: CHANZO KIKUBWA CHA AJALI KILICHOSAHAULIKA


BODABODA: CHANZO KIKUBWA CHA AJALI KILICHOSAHAULIKA

Kuna kipindi niliishi sehemu ambayo daladala za kufika kule ziliisha mida ya saa mbili za usiku na usafiri uliobaki ulikua ni pikipiki maarufu kama “bodaboda” ama labda utembee. Shughuli niliyokuwa nafanya iliniradhimu kurudi usiku mara kwa mara na sikuwa na budi kutumia bodaboda kwa usafiri. Siku moja nilipanda bodaboda ya kijana mmoja ambae kiumri anaweza kuwa kati ya miaka 17 hadi 20, naikumbuka sura yake, alikua amenyoa kiduku na hakuwa na kofia (Helmet) ya kwake mwenyewe wala ya abiria wake. Barabarani alikimbia kwa mwendo wa kasi sana kiasi cha mimi kumwambia apuguze mwendo. Alipofika sehemu ambayo alitakiwa ahamie upande mwingine wa barabara ili aende mahali nilipomuelekeza, alifanya hivyo pasi hata na kuwasha taa za kuashiria; kulikuwa na pikipiki nyingine katika upande wa pili wa barabara ambayo nayo ilikuwa katika mwendo mkali pia, ilibaki kidogo sana pikipiki zile kugongana. Yule kijana alienibeba mimi akasimama na mwenzie akasimama wakaanza kutukanana na mimi nikiwa pembeni najiuliza kama naamini katika bahati ama la! uku nikiuhisi moyo unavyokita na mikono inatetemeka, nikajua ilibakia kidogo sana nijishuhudie kwenye ajali ya bodaboda nikiwa kama abiria. Yule bwana mwingine alilalamika sisi hatukuwa tumewasha taa ya kuashiria tunavuka lakini cha ajabu yule dereva wangu alikua analalamika akisema “watu wengine bwana, hivi we huwezi kuona kama mimi navuka upunguze mwendo?mpaka niwashe taa?”.

 Image result for bodaboda ajali

Ajali za barabarani zimeongezeka sana siku hizi ukilinganisha na zamani hasa kwenye nchi za pato la chini kama yetu hii na zile za pato la kati. Kukua kwa miji na viwanda katika nchi hizi ndiko kunakopelekea kuongezeka kwa ajali hizi; namba ya vyombo vya moto imekua kwa kasi kubwa kuzidi kasi ya kuendeleza barabara bora na za kutosha. Pamoja na hali mbaya ya barabara zetu, kutotumia kinga kama vile kofia na mikanda, huduma mbovu kwa majeruhi na kutotii sharia za barabarani vinachangia matatizo yanayoambatana na ajali kwenye nchi hizi. Kiasi cha ajali kwenye nchi zinazoendelea ni zaidi ya maradufu ukilinganisha na zile zilizoendelea na tafiti zinaonesha kwamba uwezekano wa kufa kwenye ajali ukiwa hapa nchini kwetu ni mara 20 hadi 30 zaidi ya ukiwa nchini marekani ama nchi za ulaya.

Kuongezeka kwa wingi wa pikipiki hapa nchini kumekuwa na faida kwa upande mmoja ambapo vijana wamejipatia ajira ya bodaboda na usafiri huo umejidhihirisha kuwa wa haraka na nafuu ukiringanishwa na usafiri mwingine wa kukodi kama vile taxi. Kwa hapa nchini bodaboda zimeajiri vijana wengi kiasi cha kuwafanya wanasiasa kuliona kundi hili ni muhimu kwa wingi wa kura pale uchaguzi unapokuja (kama ilivyo kwa makundi mengine muhimu kwao, hupotea vinywani mwao pale uchaguzi ukishapita). Kwa upande mwingine pikipiki ndizo zinaongoza kwa ajari za barabarani hapa nchini, kwa kusababisha zaidi ya nusu ya ajali za barabarani. Tafiti moja iliyofanywa kwenye hospitali za MOI, Amana, Mwananyamala , Temeke, Tumbi na hospitali ya mkoa wa Morogoro ilionesha zaidi ya nusu ya ajali za barabarani zinazowapata watu waliofikishwa kwenye hospitali hizo zimesababishwa na pikipiki. Taffiti nyingine iliyofanywa uko katika hospitali ya rufaa ya Bugando mkoani Mwanza ilionesha hivyo pia. Ajali hizi zimeplekea vifo na ulemavu wa kudumu kwa nguvu kazi ya taifa ikizingatiwa kwamba wengi wanaopata ajali hizi ni wa umri kati ya miaka 18 na 45.

Tumekua tukishuhudia jitihada mbali mbali wakati ajali za mabasi zinapozidi nchini, jitihada hizo ni nzuri na huwa zinapelekea kupungua kwa ajali za mabasi kwa kiasi fulani. Ni vyema pia jitihada kama hizo zikawekwa kwenye upande wa pikipiki. Madereva wengi wa bodaboda wanaoumia wakati wa ajali huwa hawajavaa kofia ya kujikinga (helmet) na ni wazi kabisa kwamba karibia wote huwa hawana kofia hiyo kwa mteja wao. Isionekane tena kawaida abiria wa bodaboda kutokua na kofia, sheria kali zinahitajika sambamba na ufuatiliaji wa karibu. Wengine hubeba abiria zaidi ya mmoja (wenyewe wanaita mshikaki). Madereva wengine wa bodaboda huendesha wakiwa wamelewa pombe ama madawa mengine ya kulevya, kile kipimo cha pombe cha kupuliza kisiishie tu kwa wenye magari bali hata kwa hawa wa pikipiki maana ndio wanaosababisha ajali nyingi zaidi. Japo sijawahi kutana na chuo cha udereva wa bodaboda ila nadhani kungekuwa na mafunzo flani ambayo mtu anapitia kabla ya kuwa dereva wa bodaboda ingewasaidia kujifunza sheria za barabarani maana kwa kilichonitokea mimi hapo juu inaonesha wazi weledi wa yule dereva (labda kipo ila mimi sijui).

Pia tunaweza kupunguza kiasi cha athari pindi ajali zinapotokea. Kitu muhimu kuliko vyote kwa mtu aliyepata ajali ni huduma anayoipata kabla ya kufikishwa hospitali japo wengi huwa tunataka kumkimbiza hospitali kabla ya yote. Mara nyingi askari ndio wanahusika pale ajali inapotokea, kwa bahati mbaya inaonekana mafunzo yao hayahusishi kutoa huduma ya kwanza kwa mtu aliyepata ajali. Kuingiza mafunzo kama hayo sambamba na yale ya uaskari inaweza kupunguza namba ya watu wanaokufa kwa ajali ama athari zinazoweza kujitokeza. Pia, watu wanaokuja kusaidia baada ya ajali huwa ni wasamalia wema ambao nao huwa hawana ujuzi wa nini cha kufanya zaidi ya kuwapepea na kuwawahisha hospitali majeruhi; kuingiza mafunzo mashuleni ya nini cha kufanya mtu unapofika kuwasaidia majeruhi huenda ikawa ni njia sahihi ya kupunguza athari za ajali hizi kwa msaada kutoka kwa wasamalia wema.

Nimalize kwa kusema pindi ukijikuta unataka kuchagua chombo gani cha kupanda mbele ya vilivyopo machoni mwako kwa ajili ya usafiri, basi zingatia haya.

2 comments:

  1. Japo mafunzo yatatolewa kwa bodaboda,askari na hata kwa wananchi kwa njia ulizozipendekeza,fikra na hulka ya watanzania isipokubali kubadilika mambo haya ya ajali hayataisha.
    Ukweli ni kuwa watu wote twajua kwamba mwendo kasi na kutokuzifuata hzo sheria za barabara ndizo zaleta yote haya madhara,lakini twazifata? Hapana ndo jibu,Tubadilike.

    ReplyDelete
    Replies
    1. Ni kweli kubadili tabia ina ugumu wake ila inaweza kuharakishwa na usimamizi mkali wa sheria

      Delete