Saturday, 29 October 2016

NJIA ZA UWONGO ZA KUPUNGUZA UZITO



Wengi tunafahamu kuwa uzito uliopitiliza sio kitu kizuri kiafya. Huweza kutuongezea uwezekano wa kupata magonjwa sugu yasiyo ya kuambukiza kama vile kisukari, shinikizo la juu la damu, kiharusi, saratani za aina mbalimbali na kadhalika. Shirika la afya duniani (WHO) linakadiria kuwa mwaka 2014 kulikuwa na watu zaidi ya bilioni 1.9 waliokuwa na uzito uliozidi kiwango. Tunaweza kujua endapo uzito tulio nao ndio unaotakiwa ama umezidi kwa kuchukua uzito wetu katika kilogramu na kisha kuugawanya kwa kipeo cha pili cha urefu wetu katika mita (kurahisisha: chukua uzito wako katika kilogramu;chukua urefu wako katika mita; uzito wako gawia urefu wako; jibu ulilopata gawia tena urefu wako). Jibu likizidi 25 basi wewe uzito wako upo juu ya kiwango kinachotakiwa na unatakiwa kuanza jitihada za kuupunguza ili kupata afya njema.
 Image result for obese black women
Kwa kuwa jamii imeelimika juu ya madhara ya uzito uliozidi kiwango na kunuia kuupunguza basi wamejitokeza watu mbalimbali wanaotaka kusaidia kwa hilo, baadhi yao wapo sahihi kwa kufuata njia zilizothibitishwa kisayansi kwa kufanyiwa utafiti, na wapo ambao hawako sahihi aidha wakiwa na lengo la kuuza bidhaa zao za uwongo ama wameshindwa tu kung’amua sayansi ya nishati na chakula.

Kinachotufanya kunenepa ni kuongezeka kwa kiasi cha mafuta tunachotunza mwilini mwetu pale ambapo tumekula chakula kingi zaidi ya kile miili yetu inachohitaji kwa matumizi yake. Kizazi chetu hiki kina chakula kingi zaidi (kinacholiwa kutokana na matabaka ya kiuchumi) na kimepunguza zaidi kazi za kutumia nguvu na kuongeza shughuli zinazotufanya kukaa kwa muda mrefu kama vile runinga, simu zenye intaneti, michezo ya kielektroniki na kadhalika. Kwa kifupi ni kwamba tunanenepa pale tunapoingiza zaidi ya kutoa. Kama unafikiria vizuri utakua umekwishaona kwamba ili upunguze uzito inabidi uende kinyume na sababu iliyokufanya unenepe, yaani utoe kiasi kinachozidi.

Blog ya Afya na Kiasi inamnukuu Juma Mwaka akisema kwamba kutumia juice za matango, karoti na nyanya kila siku kwa muda wa mwezi mmoja ndio njia ya kupunguza kitambi. Hii si kweli kwani ukifanya hivi na wakati hufanyi mazoezi wala kupunguza kula vyakula vyenye nishati kwa wingi kitambi chako kitabaki palepale ama kuongezeka. Nisimlaumu sana Mwaka kwani anaonekana hata haufahamu vyema mfumo wa chakula kwani anasema “mtu anapokula chakula ni lazima kwanza kiishe kingine, vinginevyo anakuwa ametunza sumu mwilini kutokana na kuwa na mabaki mengi ya chakula cha takribani hata mwaka mmoja” na anathibitisha kwa kusema “binadamu hufa akikosa chakula kwa siku nyingi”, yeye anadhani tumbo ni kama pipa la kutunzia chakula na hajui hata mwili unatunza vipi chakula ili utumie pale unapokosa. Ukweli ni kwamba yakipita masaa manne hadi matano baada ya kula basi takribani chakula chote kinakuwa kimeondoka tumboni mwako; na pia mwili hutunza chakula kinachozidi kwanza katika ini na kingine katika hali ya mafuta, wakati ambapo hakuna chakula basi mwili huingia katika stoo zake hizi na kumeng’enya. Mwaka pia anatuambia kunywa maji ya uvuguvugu kutaondoa kitambi. Huu nao ni uwongo kwani maji ya moto hayachomi mafuta na yakishaingia mwilini yanapozwa kufanana na joto la mwili tu. Sikushangaa kusikia huyu Mwaka amefutiwa usajiri.

Mwingine anaitwa Dr. Boaz Mkumbo kwenye blog yake ya doctorboaz.blogspot.com. Huyu ameandika kuwa amesomea udaktari wa binadamu katika chuo cha Bugando na inaonekana anachanganya tiba mbadala na ya kisasa (sina neno nae kama ni ya kweli anayofanya). Moja ya huduma anayotoa ni kusafisha utumbo mpana, yaani wanaingiza kimiminika (mfano: kahawa) kwenye utumbo mpana kupitia njia ya haja kubwa. Anasema tiba hiyo inapunguza unene, kuondoa sumu(Makala yangu huko nyuma ilikataa mambo ya sumu) na kutibu magonjwa mengine. Kwanza tu labda nimwambie kwamba kuta za utumbo mpana ni safi na haziitaji kusafishwa, binafsi nimewahi kuzichungulia kwa mgonjwa aliekuwa anachunguzwa utumbo mpana kwa kamera inayoingizwa kwa mpira kupitia sehemu ya haja kubwa; na kuhusu unene: kimiminika kinachoingizwa kwenye utumbo mpana huwa kina tabia ya kufyonza maji kutoka kwenye utumbo mpana na kumfanya mtu aharishe; mtu akiharisha basi apoteza maji mengi mwilini na hivyo atapungua uzito ila baada ya siku kadhaa mwili wake utapata maji na uzito wake utarudi palepale. Lakini njia hii yaweza kuwa na madhara kwa afya pia kwani mtu anaweza kuharisha kupita kiasi, anaweza kuambukizwa magonjwa kama amoeba ama homa ya ini kama watachangia vifaa, anaweza kutobolewa utumbo mpana wake na kadhalika, kwa hiyo si salama.

Mtandao mmojawapo ambamo waweza pata taarifa sahihi za kuhusu kupunguza uzito ni www.jamiihealthtz.com. Nimalizie kwa kushauri kwamba ukisikia njia ya kupunguza uzito ambayo haihitaji jitihada, nguvu, yenye kukaa tu chini, uwezekano ni mkubwa njia hiyo ikawa ni ya uwongo.

4 comments: